Featured Posts

Monday, September 22, 2014

NI KWELI MAYAI HUSABABISHA UGONJWA WA MOYO?

UTAFITI uliofanywa nchini Marekani hivi karibuni unaonesha kuwa katika miaka ya 1950, wastani wa ulaji wa mayai ya kuku ulikuwa mayai 375 kwa mtu mmoja, lakini hadi kufikia mwaka 2007, kiwango hicho kimepungua hadi kufikia mayai 250 tu kwa mtu mmoja, ikiwa ni punguzo la asilimia 33.Sababu moja wapo ya kushuka kwa ulaji wa mayai imeelezwa kuwa, pamoja na sababu zingine, ni imani potofu kwamba mayai husababisha ugonjwa wa moyo na kwa wagonjwa wa moyo hawaruhusiwi kabisa kula mayai kwa madai kwamba yana kiwango kikubwa cha kolestro.
Hata hivyo, tafiti kadhaa zilizofanyika kuhusiana na imani hiyo potofu zimeonesha HAKUNA uhusiano wowote kati ya kuongezeka kolestro mwilini na ulaji wa mayai na kwamba mayai HAYASABABISHI ugonjwa wa moyo, iwapo mayai hayo ni halisi.
Katika siku za karibuni, tumeshuhudia kuibuka kwa ufugaji wa kuku kwa kiwango cha hali ya juu, ambapo kuku hufugwa kwa kulishwa vyakula na madawa maalum yanayowawezesha kukua ndani ya muda mfupi au kutoa mayai mengi. Hapa ndipo tatizo linapoanzia.
Wakati utafiti unaonesha kuwa mayai hayana matatizo na wala hayasababishi ugonjwa wa moyo, utafiti huo unahusu mayai ya kuku wa kienyeji ambao wamefugwa katika mazingira asilia na wanalishwa vyakula vya asili vinavyowawezesha kutoa mayai na nyama bora yenye virutubisho sahihi.
Utafiti huo umeonesha pia kuwa kuna tofauti kubwa sana ya kiwango cha virutubisho vilivyomo kwenye nyama na mayai ya kuku wa kienyeji na kuku wa kizungu.Mayai ya kuku wa kienyeji yanaonesha yana Vitamin A mara mbili mpaka tatu kuliko mayai ya kuku wa kizungu.Halikadhalika, kuku wa kienyeji wanaonesha kuwa na kiwango kikubwa cha ‘Fatty Acids’ mara mbili zaidi ya kuku wa kizungu na wakati kuna Vitamin E mara tatu zaidi ya kuku wa kizungu.
Tofauti iliyopo katika mayai ya kuku wa kizungu na kuku wa kienyeji inaweza kuonekana hata kwa macho, kwani mayai ya kuku wa kienyeji kiini chake huwa cha rangi ya chungwa iliyoiva wakati lile la kuku wa kizungu huwa jeupe na lililopauka, hata ladha yake huwa tofauti.
Jambo la msingi la kuzingatia katika suala zima la ulaji sahihi, siyo tu kwa mayai na kuku, ni kujiepusha kadiri iwezekanavyo na ulaji wa vyakula vya ‘kisasa’ na kuacha vya asili. Watu wengi hivi sasa duniani wanakula kwa wingi vyakula vya kutengeneza na matokeo yake magonjwa hatari yameongezeka. Hivyo chukuwa hatua mapema na badili mfumo wako wa maisha.

TUMEAMIA HUKU